MGANGA AJABU WA AU 1. Kimbuga Dorothy aliishi katikati mwa mbuga kubwa huko Kansas na mjombake Henry aliyekuwa mkulima pamoja na shangaziye Em, mkewe mkulima. Nyumba yao ilikuwa ndogo, kwa sababu mbao zilizotumika kuijenga ilibidi zibebwe kilomita nyingi. Kulikuwa na kuta nne, sakafu na paa, zilizounda chumba kimoja. Chumba hiki kilikuwa na jiko iliyokuwa imejaa kutu, kabati iliyowekwa sahani, meza, viti vitatu au vinne na vitanda. Mjomba Henry na shangazi Em walikuwa na jitanda kona moja, naye Dorothy kijitanda kona nyingine. Hapakuwa na dari hata, wala gorofa ya chini isipokuwa shimo ndogo iliyochimbwa ardhini, iliyoitwa shimo la kimbuga, mahali ambapo familia ingekimbia na kujificha kama mojawapo wa upepo mkubwa ungezuka.Upepo uliokuwa mkubwa kiasi cha kuvunja na kuharibu nyumba yoyote pahali popote ilipopita. Ili uingie shimo la kimbuga ulifungua mlango mdogo katikati mwa sakafu, ambapo palikuwa na ngazi iliyoshuka mpaka ndani ya shimo hii ndogo iliyokuwa na giza. Dorothy a...